Monday 23 July 2012

JK-Haikubaliki kwa mjamzito kupoteza maisha akijifungua


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa ni jambo lisilokubalika kwa mwanamke kupoteza maisha wakati akijifungua kwa sababu uja uzito siyo ugonjwa.
Aidha, rais Kikwete amesema pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali katika kupunguza vifo vya akinamama wakati wa uzazi na mipango mingine ya uzazi bora, bado tatizo linabakia kubwa na zinahitajika juhudi zaidi ili kuondokana na tatizo la vifo wakati wa uzazi.
Rais Kikwete ameyasema hayo leo, Alhamisi, Julai 19, 2012, wakati alipokutana na kuzungumza na Mtendaji Mkuu wa shirika la kimataifa lisilokuwa la kiserikali la Pathfinder International, Dkt. Purnima Mane, Ikulu, Dar es Salaam.
Amesema kuwa ni jambo lisilokubalika kabisa kwa mwanamke kupoteza maisha wakati akijifungua. “Uzazi siyo ugonjwa na kwa hakika ni jambo lisilokubalika kwa mwanamke kupoteza maisha wakati akijaribu kutoa maisha kwa binadamu mwingine. Hili ni jambo ambalo Serikali itaendelea kupambana nalo hadi kulifikisha mahali pazuri zaidi.”
Serikali imekuwa inafanya juhudi kubwa katika eneo hili lakini bado tatizo ni kubwa na zinahitaji jitihada za ziada. “Tumefanya jitihada kubwa na kupata mafanikio ya kujivunia lakini bado kazi ni kubwa.”
Takwimu za sasa zinaonyesha kuwa akinamama 578 kati ya 100,000 hupoteza maisha wakati wa uzazi, idadi ambayo imeshuka kutoka miaka minne iliyopita wakati takwimu zilionyesha kuwa akinamama 790 kati ya laki moja walikuwa wanapoteza maisha wakati wa kujifungua.
Miongoni mwa maamuzi ambayo Serikali imechukua kukabiliana na tatizo hilo ni pamoja uamuzi wa kupunguza umbali wa kufikia huduma za afya kwa kujenga zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata na hivyo kuhakikisha kuwa huduma hizo zinapatikana katika umbali usiozidi kilomita tano.
Serikali pia imeamua kuwa kila zahanati ama kituo cha afya lazima kiwe na huduma za kuhudumia wazazi na waja wazito.
Serikali pia imechukua hatua za kukabiliana na ugonjwa wa ukimwi ambao ni moja ya chimbuko kubwa la vifo vya akinamama waja wazito.
Dkt. Mane ambaye anatembelea Tanzania kwa mara ya kwanza amemsifu Rais Kikwete kwa uongozi wake katika masuala ya afya na masuala mengine. “Uongozi wako katika suala hili ni jambo linalojulikana duniani pote. Tunakushukuru sana kwa sababu wewe ni bingwa wetu na msemaji wetu mkubwa katika mapambano ya usalama wa akinamama waja wazito.”
Pathfinder International ni shirika la kimataifa lisilokuwa la kiserikali ambalo malengo yake makuu ni kushughulikia afya za akinamama na kuboresha uzazi. Katika Tanzania, Pathfinder International linaendesha miradi tisa kwa sasa katika maeneo ya ukimwi, masuala ya uzazi na uzazi wa mpango.


Habari kwa hisani ya thehabari.com

No comments:

Post a Comment